Thursday, February 28, 2013

Mtambue Mungu kama BABA by Bishop Nichodemus Shabuka



 
Kutambua ni kuelewa kufahamu na kujua, na huku kujua kuna tofauti, yupo aliyejua kwa kuelewa(Study about), yupo aliyejua kwa kusikia(Teachings), na yupo aliyejua kwa kufahamu(Experience). Ufahamu pia una viwango na hivyo viwango vinatofautiana kati ya mtu na mtu. Kumtambua Mungu kama baba ni kumfahamu, kumuelewa na kumjua Mungu, kama baba, Yaani kusoma kwa habari ya Mungu, hiyo ikihusisha Biblia na vitabu mbali mbali vya Mungu, Kufundishwa kwa habari ya Mungu hii ikihusisha sermon za kanisani, mafundisho na semina mbalimbali kwa mifumo yote ambayo wengine wanakujuza juu ya Mungu, na cha tatu ni kumjua Mungu kwa experience binafsi kama wewe.

Ubaba ni hali, sehemu na nafasi ya Mungu kwa mtu. Eneo la hali linamchukua Mungu kwa ujumla wake kama Mungu, na sehemu ni katika mapana na marefu ya Mungu ambayo mtu anaamua kumfahamu wakati nafasi inachukua cheo cha Mungu kwa mtu, heshima binafsi ambayo mtu anampa Mungu, na sio kwa maisha ya maigizo mbele za watu. Hii Jinsi mtu na Mungu wao wawili hapo hakuna Mchungaji wala mzee wa kanisa wala Mwenyekiti wa fellowship kuwatazama. Saa ambapo vyeo viko pembeni, upo wewe na Jehova peke yenu. Hapa ndio inajulikana nafasi ya Mungu kwa mtu.
Tukirudi kwenye HISTORIA  tangu Adamu hadi uchafuzi wa lugha mnara wa Babeli, Mungu alijulikana kama Mungu, historia haisemi kama kulikuwa na miungu wengine,(Mwanzo 1-11) Kuanzia Mwanzo 12 Mungu anamchagua Ibrahimu zamani akiitwa Abraham ndio Mungu anaanza kujulikana kama Mungu mwenyezi yaani Muumba mtawala maana hapa tayari wanadamu walikuwa wameshaanza kujitengenezea miungu na kuiabudu. Inaenda hivyo kuanzia Adamu hadi Yusuph. Baada ya hapo kwa Musa ndio Mungu anatoka katika jina la kiujumla na kujitambulisha kwa Musa kama Niko ambaye Niko na baadaye kusema jina la YEHOVAH, na hapo ndio anatengeneza tofauti kwa kujiteulia taifa, akijitofautisha na miungu ya mataifa Mengine. Hali hiyo imeenda kwa Israel tangu Musa mpaka Malaki hadi ujio wa Kristo. Wazo la Mungu kuwa baba wa mbinguni aliileta Yesu, huko mwanzo Mungu alijaribu kumwambia Musa Israel ni mwanangu lakini bado hili wazo halikupenya sana. Lakini Yesu katika kufundisha kwake mara kwa mara akajaribu kumsema Mungu kama Baba.
Utambulisho wa Mungu kama Baba unasogeza uhusiano zaidi toka katika hali ya utawala hadi ushirika wa karibu kabisa. Ndio maana Yesu akiwafundisha wanafunzi wake kuomba katika maneno yote kwenye lugha za binadamu ambazo angeweza kutumia, hakuchagua sifa zote ambazo kwa haraka haraka mtu angeweza kufikiria, anawaambia nanyi msalipo semeni “Baba yetu uliye mbinguni…” maana yake katika kuishi kwako bila kujali unapitia mazingira gani, katika ugumu wa aina yeyote unaokutana nao, tambua unaye baba mbinguni.

Ndio tunarudi pale kwenye Ubaba kama hali sehemu na nafasi ya Mungu kwa mtu. Hapo kuna mambo muhimu ya kuzingatia moja ni kumtambua Mungu kama,
Mwanzilishi(Initiator) Mwanzo 1:1-3. Ufunuo 1:8. Alfa na Omega, Wa kwanza na wa mwisho.  Hebrews 12:2 “Mwanzilishi na mwenye kutimiliza imani yetu. Unapomtambua Mungu kama mwanzilishi, kila ambacho unaanzisha kwenye maisha yako utamshirikisha na kumhusisha. Na hapa level ya mahusiano yaliyopo kati yako na Mungu ndio itategemea level ya uhusishwaji na ushirikishwaji Mungu atapewa kwenye maisha ya mtu. Wapo watakao mpa kila kitu atawale na wapo watakao mpa baadhi ya vitu. Hii haiwezi kufanana, ni experience ya tofauti kwa kila mtu. Mungu Alishakupa nafasi ya kuamua Mwanzo 1:26, hawezi kukulazimisha mambo yako mpaka umemhusishe na hiyo ndio kutambua mamlaka na nafasi aliyonayo. Kwa kiwango hicho hutakurupuka kufanya biashara wala harusi bila kutafuta uso wa Mungu na kibali juu ya jambo hilo.

Ukimpa Mungu nafasi kama Baba na Muanzilishi, hutaogopa kuanza jambo maadamu umemuomba na ukapata amani, hata kama ulimwengu mzima utakuwa kinyume nawe bado hutaogopa ikiwa Mungu peke yake atasimama upande wako. Bwana akiwa upande wetu, nani aliye juu yetu.
Mtoaji(Provider) Unapomtambua Mungu kama Baba wa Mbinguni akupaye wewe mkate wa kila siku, huta hofu hata ukisikia njaa inakuja maana kwa kumtegemea huku ukitumia akili atakupa mbinu za kuhifadhi chakula na kuepuka njaa. Kama jinsi alivyompa ufahamu Yusuph nakujua cha kufanya ili kukabili miaka saba ya shibe na miaka saba ya njaa. Roho ya ubora ipo juu ya wana wa Mungu. Kuna neema ya hekima na ujuzi pamoja na ufanisi mara kumi zaidi ya waganga na wachawi, wapiga bao na wanajimu. Mungu ajuaye mwisho kabla ya Mwanzo anachohitaji ni nafasi kwenye maisha yako akustareheshe kwa raha na utele maana ndivyo alivyokuumbia. Mruhusu Mungu kwenye maisha yako ili akubadilishe na kukuingiza kwenye mfumo wa utawala wake.

Mlinzi(Protector). Isaiah 49:16.  Kama  vile baba alivyona wajibu wa kuilinda familia yake, mke na watoto wake, naye Mungu anahusika kutoa ulinzi kwa watoto wake. Unapompa nafasi kama Baba kwako anachukua jukumu la kukulinda moja kwa moja kwa njia ya imani. Anasema amekuchora kwenye vitanga vya mikono yake, hakuna kinachokutokea ambacho hajui, anakulinda kama mboni ya jicho lake. Kumb 32:10  na Zakaria 2:8.  Hivi ndivyo Mungu anakulinda kama Baba, ukijua haya lazima utatembea kifua mbele pasipo kuogopa yanayojili au kutokea ulimwenguni. Biblia inasema elfu wataanguka upande wako wa kushoto na makumi elfu upande wako wa kulia bali wewe mabaya hayata kupata, Kwanini? Kwasababu Mungu atakushika kwa mkono wa kuume wa nguvu zake.

No comments:

Post a Comment