Wednesday, September 18, 2013

Uchumba hadi Ndoa: Ni Vizuri Watarajiwa kukubaliana juu ya mipaka watakayokuwa nayo kwa Ndugu wa pande zote mbili



 

Shalom Mtu wa Mungu, leo nakuletea somo muhimu sana juu ya kukubaliana na mwenzi wako jinsi mtakavyokuwa mnaishi na ndugu zenu, yaani wakwe kwa upande wa mwanaume na mwanamke pia.

Ni muhimu mkaweka  msingi mapema maana wazazi na ndugu za pande zote mbili ni muhimu sana sana kwenu wala hawahitajiki kuupuuziwa ila tu msipoweka mipaka inaweza kuleta shida kubwa sana katika maisha yenu ya huko mbele mtakapokuwa mmefunga ndoa.

Wakati mwingine ndugu za pande zote mbili wamekuwa wakijisahau na kufikiri wana nafasi ya kuamua juu ya maisha yenu kama wanandoa. Lakini katika Biblia tunaona kuna mifano mingi jinsi wanandoa walivyoishi vizuri na wakwe zao kukawa na uhusiano mzuri kati ya wakwe na mkwe kama Ruth na Naomi walivyopendwa na kuishi vizuri na wakwe zao.

Lakini pia tunaona jinsi ambavyo Mfalme Daudi alivyopata shida na baba mkwe wake Mfalme Sauli hadi Sauli akataka kumuua Daudi.


Mahusiano mabaya kati ya mkwe na wakwe yanaweza kusababisha wanandoa kuishi kwa shida kubwa sana na mara nyingine imesababisha ndoa kuvunjika kabisa na kuleta chukizo mbele za Mungu.

Sasa ili kuepusha hayo ndio maana tuko hapa leo kukuambia kwamba msije mkajisahau mkaongelea tu jinsi mtakavyojenga Masaki au Kibada bila Kuzungumzia jambo hili mapema maana kama usipoliweka sawa hutaishi kwa Raha, Ninaposema Ndugu hapa namaanisha ni mama,baba,kaka,dada,shangazi,mjomba,bibi ,babu na ndugu wengine wa kwako wewe au wa mwenzi wako pamoja na uzao wao.

Zingatieni yafuatayo ili kuepusha hiyo migogoro inayosababishwa na ndugu;

 

1. Zungumza na Mwenzako

Mzungumze jinsi mtakavyoweka mipaka kwa ndugu zenu wote itayaepusha ndugu kuingilia mahusiano yenu

Kwa mfano sikilizeni ushauri kutoka kwa wakwe maana pia ni mzuri sana kwasababu wao kwanza wameona mengi kuliko nyie ila kabla ya kufanya maamuzi make chini mkubaliane lipi mfanye au lipi mliache kwanza. Kwa kufanya hivyo mtakuwa na mahusiano mazuri maana mmeshirikishana kwenye maamuzi juu ya mashauri mliyopata.                             

Ni hatari sana ukapigiwa simu na mama au baba au mjomba wako kwamba mwanangu kuna kiwanja huku Mwabepande wewe kwa vile ulikuwa na hela Bank ukaikimbizia huko ukanunua bila kumuambia mwenzako, halafu baadae ajue kwamba umemruka katika maamuzi . Mshirikishe maana ndio unategemea kuishi naye anaweza kukupa ushauri mzuri ambao utaweza kupata kitu kizuri na cha thamani na saa nyingine kukuepusha na hasara.


2. Muwe wazi kwa Ndugu na ishi nao kwa Akili

Inategemea na ndugu zenu wakoje na wanawachukuliaje, kuweni tu wawazi kwamba Bwana ninavyomjua mchumba wangu hili jambo hatalikubali labda uniruhusu nimwambie kwanza tusikie mawazo yake.

Ukimshirikisha kwanza kabla hujaamua atajisikia vizuri na anaweza kuruhusu mfanye chochote na ndugu.

Kama mna ndugu ambao si warahisi sana kuelewa wanapenda uchokozi ishi nao kwa akili jifunze kunyamaza ni silaha kubwa sana.

Ukinyamaza na kuongea na mwenzako kwamba nimenyamaza kwasababu naona nikiongea naweza kuchochea moto zaidi atakuelewa kwamba hujadharau ndugu zake na mtaweza kuomba Mungu aseme na hao ndugu waweze kuwaelewa na kuwachukulia.

Kuwa wazi kwa ndugu kwamba kwasasa hatuwezi kufanya maamuzi haya ya kifedha kwasababu hatuko vizuri kifedha labda kwasababu tunajiandaa na maandalizi ya harusi au mambo mengine ambayo nyie mmeona ni ya muhimu zaidi.

 

 

3. Badilika

Kama ndugu wa mwenzako wanalalamikia tabia fulani ambayo unayo jichunguze na ifanyie kazi ubadilike labda una dharau, majivuno na kiburi ongea na Roho Mtakatifu atakushauri ni wapi ubadilike na atakuwezesha kubadilika, Mungu anabadilisha watu san asana kuliko unavyodhani ila hawezi kufanya mpaka umwachie.

Ila kama wanataka ubadilishe kitu ambacho kiko nje ya uwezo wako na kiko nje ya mapenzi ya Mungu , zungumza na mwenzako mliombee hilo maana watakuwa tu wanataka kuwavuruga au kutaka mjisikie vibaya. Maana kuna rafiki yangu aliambiwa huyo mwenzi wako hatumtaki kwasababu anatoka kabla fulani sasa hebu niambie je huyo dada angebadilisha Kabila wapendwa ilimhitaji Mungu aingilie kati na kama ikiwa ngumu sana mumuone mchungaji wenu atawashauri au atazungumza na hao wazazi.

 

 

4. Watarajiwa mshirikishane kila kitu na kupendana kwa Dhati

Kama nilivyokwisha kusema huko nyuma watarajiwa inabidi muunganishe na Upendo wa hali ya juu, Maana Neno linasema Upendo huficha wingi wa Dhambi.

Kama mwenzako anakupenda hataona madhaifu yako bali atakusaidia kwa upendo uweze kubadilika na sio kuungana na ndugu zake na kukusema na kukukashfu.

Shirikianeni kwa upendo ili kuwa na bond, ndugu wakijua mnapendana kwa dhati watakosa nafasi ya kuwahangaisha na Maneno ya mafarakano.

 

Mungu akubariki sana unapojindaa kuingia katika Hatua hii ya Ndoa, na hata kama huna Mchumba soma haya na Omba Mungu kwa Imani ujue kwamba yuko mtu wako aliyekuandalia kwahiyo usikate tamaa kaa mkao wa Kuoa au Kuolewa muda si Mrefu Mungu anakutembelea, Aminaaaaaaaaaaaa!

 

 

Endelea kusoma Rejoice and Rejoice Mambo mazuri yanakuja, na soma masomo ya huko nyuma yako masomo ya muhimu sana ya kukuandaa kuwa mwanandoa mwenye ushindi Katika Kristo Yesu.

 

 


No comments:

Post a Comment