Tuesday, April 15, 2014

Uchumba hadi Ndoa: Jifunze kuchukuliana na Mwenzi wako



Hata Mungu anafurahi ndoa inapokuwa na furaha na raha
 
Karibu katika masomo haya ya Uchumba hadi ndoa ,yanayoletwa kwenu na Mshauri wako wa Mahusiano na Ndoa.

Kwanza nikuombe sana radhi kutorusha masomo haya kwa muda mrefu lakini sasa kwa uwezo wa Mungu tutakuwa tunaendelea na masomo yetu kila wiki.

Kwahiyo uweke katika kalenda na kumbukumbu zako kila siku ya Jumanne tutakuwa na masomo haya….Karibu tuendelee..

Leo naomba nizungumzie kitu ambacho ni muhimu sana kwa mahusiano na ndoa pia. Unapojiandaa kuingia katika ndoa unapaswa kujiandaa jinsi utakavyokwenda kuishi na mwenzi wako. Maana uhusiano unaouendea sio kama ule uliokuwa nao na Baba, Mama, kaka, dada au bibi yako ni Zaidi sana mpendwa, unaingia katika uhusiano wa karibu wa ndani mtu ambaye utalala naye kitanda kimoja kila siku na wakati.
Mwenzi wako wa ndoa ni mtu wa karibu hata kama hujisikii kumuona

Mtu ambaye iwe jua iwe mvua utakuwa unamuona.

Mtu ambaye hata kama hujisikii kuongea na mtu siku hiyo atakuongelesha

Mtu ambaye hata kama hujisikiaa kumuona atakuwepo hapo na utamuona

Ni mtu ambaye lazima uwe naye karibu hata kama siku hiyo amekukwaza sanaa

Ndio maana nikaona kuna umuhimu wa kuwa na masomo haya maana mengi yametokea kama tunavyoona katika jamii sasa, talaka sasa inatolewa tu kirahisi rahisi tu, zamani nilipokuwa mdogo kiukweli kabisa nilikuwa sijui kama kuna talaka huo ndio ukweli wangu. Mungu alinipa neema ya kuwa katika mazingira hayo, sasa nilipokuwa na nikawa mjini ndipo nikasikia hiyo sentensi lakini bado niliona kama ni ya kundi fulani tu lakini nakuambia sasa inaogopesha maana imeingia kanisani. Katika kutafakari haya Mungu akanipa mzigo huu niseme na nyie watu wake kwamba NDOA BILA TALAKA INAWEZEKANA,Amen..

Haya tuendelee na Somo letu sasa, kuhusu kuchukuliana ni hali ya kumuelewa mwenzako pale anapofanya kitu ambacho hakikufurahishi au usichokipenda. Lakini kuchukuliana sio kupuuzia au kudharau naomba nitofautishe maana wengi wanapuuza au kudharau mambo wenzao wanayoyafanya hiyo nayo yaweza kuleta shida.

Ukimchukulia mtu utaona mazuri badala ya mabaya, utaona upande wake mzuri Zaidi ya ule mbaya. Najua utaniuliza kuna mtu mbaya kweli? Ni kweli kabisa kila mtu ana sehemu mbili za maisha ana upande chanya na hasi au ana upande wa mazuri na madhaifu , kila mwanadamu ana pande zoote hizo wala usije ukafikiri ni wewe mwenyewe.

Zamani nilikuwa nasema nitaolewa na mchungaji maana wao ni watumishi wa Mungu hawana shida, lakini hata awe askofu, Nabii, Mpwakwa Mafuta etc, ana pande mbili nzuri na madhaifu maana yeye ni mwanadamu. Ni Mungu tu anatupa nguvu ya kushinda katika madhaifu yetu.

Sasa kama mwenzako atakuwa na kitu ambacho hakikufurahishi na umeshamwambia weee na habadiliki ni jukumu lako Kumuelewa , Kumuombea na KUMCHUKULIA yaani hapo utakuwa na ndoa yenye ushindi hapa duniani, furaha na raha zitakuwa ni sehemu ya maisha yenu, Amen..

Kama mwenzako ana tabia za Ujeuri, mwelewe kwanza hii tabia imeletwa na nini maana kuna wakati unaweza kuwa wewe ndio chanzo cha tabia mbaya kwa mwenzako, lakini pia nyingine ni malezi aliyokuwa nayo.

Kuna mtu ninamjua amelelewa katika familia yenye wakaka wengii sana, yeye akiwa mtoto wa kike peke yake kwahiyo hata kuongea na vitabia fulani ni vya kiume kiume, sasa mume atakayemuoa asipomuelewa huyu dada itakuwa ni mtihani maana anaweza kuongea kitu cha kisela sela mume akaona hivi nimeoa mwanaume mwenzangu au? Lakini atakapoelewa kwamba hii ni adhari ya mazingira mwenzi wangu aliyokulia itakuwa ni faida kwa wote maana ataweza kumsaidia mwenzake na pia atamchukulia pindi tabia ile ya kibabebabe na kisela inajiinua lakini asipomuelewa hiyo ndoa itakuwa na shida sana.

Lakini pia ukiona mwenzako anashindwa kukuelewa na wewe inabidi u-efatha (funguka) mwambie mbona mimi naona kawaida kwasababu nilizoea kuongea hivyo na ndugu zako sasa sikuwahi kuambiwa kama ni shida basi kama kwako ni shida nitaacha naomba Mungu anisaidie.

Sasa kama wewe unajifanya ni mtu wa sheria sheria unataka mwenzako atembelee katika chaki utapata shida sana katika ndoa, kwasababu kwanza hakuna mtu aliye mkamilifu na pili mwenzako ataishi kwa uwoga sana na wewe atakuogopa mnoo. Sasa akikuogopa ni hatari kwa ndoa maana kuna mambo mengi ya muhimu yak wake hutayajua na anaweza kujaribiwa kuwa na marafiki wa  nje..

Kuna mtu alisema yeye alilelewa katika mazingira ya mpangilio sasa alivyooa mke wake akawa ni mtu ambaye kwakweli anaweka vitu hovyohovyo, sasa yule kaka akawa anakwazika sana sana akawa anamwambia mwenzake wewe ni mtu wa aina gani unakuwa haufanyi vitu kwa mpangilio? Mwenzake naye akawa anakwazika mbona huyu ana Maneno makali mbona mimi nimekaa kwetu miaka 20 plus hakuna hata ndugu yangu mmoja alinisema hivyo… sasa hilo swala likaleta shida kubwa katika ndoa hiyo, kukawa hakuna maelewano ndani ya ndoa , ndio huyu mkaka kwa hekima ya Mungu akajitenga akamuomba Mungu , ndipo Mungu akamfundisha kuchukuliana na mwenzake, na ndoa ikasalimika. Niliweza kumuona akitoa ushuhuda hapa nimefupisha ila kuchukuliana kuliokoa sana ndoa yao.

Kama ndio mko katika uchumba anza kumuomba Mungu akusaidie uweze kuchukuliana na mwenzako.

Namna ya kujifunza Kuchukuliana na mwenzi wako;

Ili kuchukuliana na wenzako iwe sehemu ya maisha yako unahitaji kujifunza kwa njia zifuatazo;

1.      Anza kuchukuliana na ndugu zako, wadogo zako na jamaa zako

2.      Chukuliana na wanafunzi wenzako kama uko chuo

3.      Jifunze kuchukuliana na room mate wenzako kama uko chuo

4.      Chukuliana na wapangaji wenzako kama umepanga nyumba ya watu wengi

5.      Chukuliana na washirika wenzako kanisani

6.      Jinfunze kuchukuliana na wafanyabiasha wenzako

7.      Popote ulipo ukatukatana na mtu akakukwaza jitahidi kumchukulia

 

Ukijifunza hayo utakuta umeifanya ikawa tabia yako yaani utajikuta unawachekea na kuwafurahia wale wanaokukwaza na utaishi maisha ya ushindi ambayo Mungu ametukusudia tuishi hapa duniani.

 

Halleluya tukutane tena wiki ijayo katika masomo yetu haya ya Mahusiano na Ndoa, endelea kututembelea lengo letu ni kuona watu wanaishi kama Mungu anavyotaka tuishi, kwa msaada wa Mungu tunajua Ndoa na Mahusiano mazuri yanawezekana, Haleluyaaaaaaaaaaaaaaa!!


Endelea kutembelea Rejoice and Rejoice Mambo mazuri yanakuja..
 

No comments:

Post a Comment