Monday, December 19, 2016

MAOMBI YA KUFUNGUA MALANGO NA MILANGO - SEHEMU YA 6

AINA TANO ZA FUNGUO ZA KUFUNGUA MALANGO NA MILANGO

Na Mchungaji Florian Katunzi - EAGT City Center

UFUNGUO WA TANO

NGUVU ZA ROHO MTAKATIFU

Neno “Nguvu” kwa lugha ya Kigiriki ni (dunamis) ina maana ya zaidi ya Nguvu au Uwezo wa kawaida. “Inaashiria hasa nguvu iliyo katika utendaji wa ki-Mungu, hii ni nguvu zaidi ya nguvu.
(Dunamis is not just any power; it is miraculous power or marvelous works. Dunamis can also refer to “Moral power and excellence of soul according to the Greek lexicon). Nguvu ya Roho mtakatifu inajumuisha mamlaka ya kutoa pepo wachafu na upako wa kuponya magonjwa. Roho mtakatifu ndiye ufunguo wa kumshinda adui shetani na kazi zake. Roho mtakatifu ni zaidi ya nguvu ama uweza. Katika maandiko matakatifu, Yesu kristo alionyesha unafsi wa Roho mtakatifu kwa kumwongelea kama nafsi ambapo alisema; “Lakini yeye atakapokuja, huyo Roho  wa kweli, atawaongoza awatie kwenye kweli yote; kwa maana hatanena kwa shauri lake mwenyewe, lakini yote atakayoyasikia atayanena, na mambo yajayo atawapasha habari yake.” Yohana 16:13

Kimsimgi tunajifunza kwa Yesu Kristo kabla ya kuanza huduma yake hapa ulimwenguni, alipokwisha kubatizwa na Yohana mbatizaji, wakati anaomba mbingu zilifunguka Roho mtakatifu akashuka juu yake kwa Nguvu tangia hapo maandiko matakatifu yanathibitisha “Ikawa watu wote walipokwisha kubatizwa, na Yesu naye amebatizwa, naye anaomba, mbingu zilifunuka; Roho mtakatifu akashuka juu yake kwa mfano wa kiwiliwili, kama hua, sauti ikatoka mbinguni wewe ndiye mwanangu mpendwa wangu ninyependezwa nawe.” Luka 3:21-22

Tunajifunza katika maandiko haya yakuwa Nguvu ya Roho mtakatifu haishuki kwa mtu hivihivi mpaka awe anaomba. Lakini wako wakristo wengi wanaotaka kujazwa Roho mtakatifu wakati hawana maombi katika maisha yao. Maombi ufungua mbingu zimfungukie mwombaji. Baada ya Yesu kristo kujazwa Roho mtakatifu, maandiko matakatifu yanashuhudia wazi yakuwa aliongozwa na Roho muda wa siku arobaini katika maombi. “Naye Yesu, hali amejaa Roho mtakatifu, alirudi kutoka Yordani, akaongozwa na Roho muda wa siku arobaini nyikani.”  Luka 4:1

Pia yunajifunza ili milango na malago ya ukombozi wa mwanadamu yapate kufunguliwa ilibidi Roho mtakatifu ashuke kwa nguvu na uweza mkuu ili kumfunika mwanamwali bikra apate uwezo wa kubeba mimba pasipo kukutana na mwanamume kwa jinsi ya kibinadamu.
“Mwezi wa sita, malaika Gabrieli alitumwa na Mungu kwenda mpaka mji wa Galilaya, jina lake Nazareti, kwa mwanamwali bikira aliyekuwa ameposwa na mtu, jina lake Yusufu, wa mbari ya Daudi; na jina lake bikira huyo ni Mariamu. Akaingia nyumbani kwake akasema, Salamu, uliyepewa neema, Bwana yu pamoja nawe. Naye akafadhaika sana kwa ajili ya maneno yake, akawaza moyoni, Salamu hii ni ya namna gani? Malaika akamwambia, Usiogope, Mariamu, kwa maana umepata neema kwa Mungu. Tazama utachukua mimba na kuzaa mtoto mwanamume, na jina lake utamwita Yesu. Huyo atakuwa mkuu, ataitwa Mwana wa aliye juu, na Bwana Mungu atampa kiti cha enzi cha Daudi, baba yake. Ataimiliki nyumba ya Yakobo hata milele, na ufalme wake utakuwa hauna mwisho. Mariamu akamwambia malaika, Litakuwaje neno hili, maana sijui mume? Malaika akajibu akamwambia, ROHO MTAKATIFU ATAKUJILIA JUU YAKO, na nguvu zake aliye juu zitakufunika kama kivuli; kwa sababu ya hicho kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, mwana wa Mungu.”

Roho mtakatifu akishuka kwetu huja na nguvu zake aliye juu katika Uwezo na nguvu za Roho Mtakatifu, tunavishwa uwezo wa kuangusha ngome zote zilizofunga Malango na Milango yetu ya Baraka za kiroho na kimwili, ndiyo maana Bwana Yesu kristo alisema, Mtapokea nguvu akisha kuwajilia Roho Mtakatifu. Mkristo nguvu yako haimo katika vitu vya upako kama vile; mafuta ya upako, maji ya upako, sabuni za upako, chumvi ya upako, kitambaa cha upako, udongo wa upako, kiganja cha nabii wa upako nambo yafananayo na hayo yanayoibuliwa kila kukicha katika ibada zilizotungwa kwa akili za binadamu. Ndugu mpendwa katika kristo yachunguzeni maandiko vema; mpate kuijua kweli inayoweza kuwawekeni huru mbali na mateso. Tukiwa na msimamo thabiti wa kiimani yatupasa kuliamini Neno la Mungu sio maneno ya watu, watawaijieni kwa mfano wa wanakondoo lakini ndani ni mbwa mwitu wakali. Maagizo ya Yesu Kristo aliye mwanzilishi wa huduma hii iliyokubwa na bora anasema;  Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.” Matendo 1:8
Yesu kristo aliwaambia wanafunzi wake msitoke Yerusalemu bali mwingojee nguvu ya Roho mtakatifu, ambayo kwa hiyo watatenda kazi ya kufungua waliofungwa. Maana pasipo huyo Roho mtakatifu hakuna atakayeweza. Tunaona akina Petro na Yohana baada ya kupokea Nguvu ya Roho mtakatifu waliweza kunena habari za Kristo Yesu na ufalme wake kwa ujasiri na nguvu. Hata wengi walistaajabu walipoona ujasiri wao. “Ndipo Petro akijaa Roho mtakatifu, akawaambia, enyi wakubwa wa watu na wazee wa Israeli … wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine katika mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo. Basi walipoona ujasiri wa Petro na Yohana, na wakajua ya kuwa ni watu wasio na elimu, wasio na maarifa wakastaajabu wakatambua ya kwamba walikuwa pamoja na Yesu.” Mdo 4:8-13

Kwa hiyo Roho mtakatifu akiwa kwa mtu hujidhihirisha kwa madhihiriho ya ishara, miujiza na maajabu ambayo huwastaajabisha wengi wayaonapo. Roho mtakatifu uhuisha nafsi zetu na miili yetu toka kwenye mafungo ya giza kwa kutufungulia malango na milango. Tunajifunza kwa Lazaro alipougua, akafa, akazikwa kwa muda wa siku nne alikuwamo kaburini lakini kwa nguvu za Roho mtakatifu Yesu alipaza sauti yake akamwita Lazaro toka kwa wafu akawa hai tena. Hata sasa Roho mtakatifu bado anatenda kazi kwa wote waaminio maana tukimwita katika Kristo Yesu ushuka kuokoa na kuponya wengi. Hata kama lipo kaburi limefunga maisha yako ya kiroho na kimwili kwa uweza na nguvu za Roho mtakatifu sharti ufunguliwe. (Through Power of Holy Ghost we Force out evil spirit). Maandiko yanasema katika injili ya Yohana;Basi mtu mmoja alikuwa hawezi, Lazaro wa Bethania, mwenyeji wa mji wa Mariamu na Martha, dada yake. Ndie Mariamu yule aliyempaka Bwana marhamu, akamfuta miguu kwa nywele zake, ambaye Lazaro nduguye alikuwa hawezi. Basi wale waumbu wakatuma ujumbe kwake wakisema, Bwana, yeye umpendaye hawezi. Naye Yesu aliposikia, alisema, Ugonjwa huu si wa mauti, bali ni kwa ajili ya utukufu wa Mungu, ili mwana wa Mungu atukuzwe kwa huo. Naye Yesu alim,penda Martha na umbu lake na Lazaro. Basi aliposikia ya kwamba hawezi, alikaa bado siku mbili pale pale alipokuwapo. Kisha, baada ya hayo, akawaambia wanafunzi wake, Twendeni Uyahudi tena. Wale wanafunzi wakamwambia, Rabi, juzi juzi tu Wayahudi walikuwa wakitafuta kukupiga kwa mawe, nawe unakwenda huko tena? Yesu akajibu, Je! Saa za mchana si kumi na mbili? Mtu akienda mchana hajikwai; kwa sababu aiona nuru ya ulimwengu huu. Bali akienda usiku hujikwaa; kwa sababu nuru haimo ndani yake. Aliyasema hayo; kisha baada ya hayo, akawaambia, Rafiki yrtu, Lazaro amelala, lakini ninakwenda nipate kumwamsha. Basi wale wanafunzi wakamwambia, Bwana, ikiwa amelala, atapona. Lakini Yesu alikuwa amenena habari ya mauti yake; nao walidhania ya kuwa ananena habari ya kulala usingizi. Basi hapo Yesu akawaambia waziwazi, Lazaro amekufa. Nami nafurahi kwa ajili yenu kwamba sikuwako huko, ili mpate kuamini; lakini na twendeni kwake. Basi Tomaso, aitwaye pacha, akawaambia wanafunzi wenziwe, twendeni na sisi, ili tufe pamoja naye. Basi Yesu alipofika, alimkuta amekwisha kuwamo kaburini yapata siku nne. Na Bethania ilikuwa karibu na Yerusalemu, kadri ya maili mbili hivi, na watu wengi katika Wayahudi walikuwa wamekuja kwa Martha na Mariamu, ili kuwafariji kwa habari ya ndugu yao. Basi Martha aliposikia kwamba yesu anakuja, alikwenda kumlaki, na mariamu alikuwa akikaa nyumbani. Basi Martha akamwambia Yesu, bwana, kama ungalikuwapo hapa, ndugu yangu hangalikufa. Lakini hata sasa najua ya kuwa yo yote utakayomwomba Mungu, Mungu atakupa. Yesu akamwambia, ndugu yako atafufuka. Martha akamwambia, najua yakuwa atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho. Yesu akamwambia, mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi, naye kila aishie na kuniamini hatakufa kabisa hata milele. Je! Unayasadiki hayo? Akamwambia, Naam, Bwana, mimi nimesadiki ya kwamba wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu, yule ajaye ulimmwenguni. Naye alipokwisha kusema hayo, alikwenda zake, akamwita umbu lake Mariamu faraghani, akasema, Mwalimu yupo anakuita. Naye aliposikia aliondoka upesi, akamwendea. Na Yesu alikuwa hajafika ndani ya kijiji, lakini alikuwa akalipo palepale alipomlaki Martha. Basi wale Wayahudi waliokuwapo na Mariamu nyumbani, wamfariji, walipomwona jinsi alivyoondoka upesi na kutoka, walimfuata, huku wakidhani ya kuwa wanakwenda kaburini ili alie huko. Basi Mariamu alipofika pale alipokuwapo Yesu, na kumwona, alianguka miguuni pake, akamwambia, Bwana, kama ungalikuwapo hapa, ndugu yangu hangalikufa. Basi Yesu alipomwona analia, na wale Wayahudi waliofuatana naye wanalia, aliugua rohoni, akafadhaika roho yake, akasema, Mmemweka wapi? Wakamwambia, Bwana, njoo utazame. Yesu akalia machozi. Basi Wayahudi wakasema, angalieni jinsi alivyompenda. Bali wengine wao wakasema, je! Huyu aliyemfumbua macho yule kipofu, hakuweza kumfanya na huyu asife? Basi Yesu, hali akiugua tena nafsini mwake, akafika kwenye kaburi. Nalo lilikuwa ni pango, na jiwe limewekwa juu yake. Yesu akasema, Liondoeni jiwe. Martha, dada yake yule aliyefariki, akamwambia, Bwana, ananuka sasa; maana amekuwa maiti siku nne. Yesu akamwambia, Mimi sikukuambia ya kwamba ukiamini utauona utukufu wa Mungu? Basi wakaliondoa lile jiwe. Yesu akainua macho yake juu, akasema, baba, nakushukuru kwakuwa umenisikia. Name nalijua ya kuwa wewe wanisikia siku zote; lakini kwa ajili ya mkutano huu wanaohudhuria nalisema haya, ili wapate kukusadiki kwamba ndiwe uliyenituma. Naye akiisha kusema hayo, akalia kwa sauti kuu, Lazaro, njoo huku nje. Akatoka nje yule aliyekufa, amefungwa sanda miguuni na mikononi, na uso wake amefungwa leso. Naye Yesu akawaambia, Mfungueni, mkamwache aende zake.” Yohana 11:1-44
Roho mtakatifu huleta uzima badala ya mauti; akatoka nje maana yake, akahuwishwa Lazaro toka kwa wafu japo alikuwa amekufa na ameoza. Ijapokuwa alikuwa ananuka, nguvu ya Roho Mtakatifu iliposhuka juu yake aliyekuwa katika hali ya kufa ikamwinua Lazaro toka kwa wafu akawa hai tena. Ni vema kila mmoja aliyeamini kutambua kuwa Roho mtakatifu ni Ufunguo unaotoa nafsi nyingi katika mafungo ya giza. Kwa nguvu za Roho mtakatifu hata kazi zetu za kimwili zaweza kuhuishwa inaweza kuwa Biashara, Kazi, Elimu vyote vilivyozikwa na kufishwa kuwa hai tena. Kama BWANA alivyonena kwa kinywa cha nabii Ezekieli na kusema; “Nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi BWANA, nitakapoyafunua makaburi yenu, na kuwatoa ninyi katika makaburi yenu, enyi watu wangu. Nami nitatia roho yangu ndani yenu, nanyi mtaishi, nami nitawawekeni katika nchi yenu, nanyi mtajua ya kuwa mimi, BWANA, nimesema hayo, na kuyatimiza, asema BWANA.” Ezekieli 37:13-14

Kwa nguvu za Roho mtakatifu sharti malango na milango vifunguliwe ndani mwa maombi sio nje ya maombi kwa kuwa tunapomlilia Mungu na kumwita, yeye hushuka na kutufungua mafungo yetu yote. “Naye Yesu akiisha kupaza sauti tena kwa nguvu, akaitoa roho yake. Na tazama pazia la hekalu likapasuka vipande viwili toka juu hata chini, nchi ikatetemeka; miamba ikapasuka, makaburi yakafunuka; ikainuka miili mingi ya watakatifu waliolala, nao wakiisha kutoka makaburini mwao, baada ya kufufuka kwake, wakauingia mji mtakatifu, wakawatokea wengi.” Mathayo  27:50-57

Nchi ilitetemeka
Wakuu wa anga lazima watetemeke maana Roho Mtakatifu ni nguvu iliyo juu ya yote lazima Wakuu wa nchi washushwe, Wakuu wa giza washushwe, Wakuu wa majini washushwe katika viti vyao kwani Kila goti lazima lipigwe mbele ya Kristo Yesu Mwokozi. 

Miamba ilipasuka
Wako watu wamefungwa nafsi zao katika miamba na majabali mazito, lazima ipasuke ili wote waachiliwe waliofungwa vifungo kwenye miamba kupitia nguvu ya Roho mtakatifu.

Makaburi yakafunuliwa
Kaburi ni kifuniko kibaya sana kinachotesa wengi. Wengi wanafunikwa makaburini kupitia makafara ya tambiko. Kwa nguvu za Roho Mtakatifu miili mingi ya watakatifu waliofungwa na nguvu ya kaburi watainuka.

Kama pazia la hekalu lilivyopasuka, ndivyo kila kizuizi kilichowekwa katika maisha yako ya kiroho na kimwili kitapasuka toka juu mpaka chini. Huu ndio ulikuwa mwisho wa Agano la kale na kuwa mwanzo wa Agano jipya. Katika Kristo Yesu yakale sasa yamepita tazama yamekuwa mapya. Katika ulimwengu wa Roho watu wengi wamefungwa na mapazia ya mabibi na mababu zao, mapazia ya kiganga na kichawi, mapazia ya mizimu na matambiko, lazima tuwafungue watu wa Mungu mapazia hayo ndani mwa maombi haya ya kufungua milango na malango. Yesu akasema mfungueni sanda mwache aende zake. Ikiwa na maana Lazaro alipofufuka alitoka kaburini akiwa amevaa sanda (vazi la wafu) ndiyo maana Kristo Yesu aliagiza avuliwe hilo vazi yaani sanda ndipo aachwe huru aende zake. Hapa tunapata siri nzito ya kiroho ya kuwa wako wakristo wengi waliookolewa toka katika mafungo ya giza lakini hawajahamishwa na kuingizwa katika ufalme wa mwana wa pendo lake. Ni jukumu letu watumishi wa Mungu kufanya maombi na maombezi ya kuwafungua watu baada ya kuamini. Maana KWELI ya Mungu kupitia Neno ndiyo inayomuweka mtu huru mbali na mateso. Ni muhimu sana tukafundisha na kuombea sawasawa na Neno la Mungu. Maana wako wanaodhania ya kuwa baada ya kuokoka vita vyao vimeisha kumbe wokovu ndio mwanzo wa vita vya kiroho na kimwili. Kwa mantiki hiyo ndiyo maana Bwana Yesu akawaambia wanafunzi wake; “Kesheni mwombe, msije mkaingia majaribuni, roho i radhi ila mwili ni dhaifu.”  Marko 14:38

Hata wana wa Israaeli walipokwisha kuokolewa toka utumwani Misri kwa nguvu na uweza mkuu, tunajifunza kwao jinsi walivyokutana na vipingamizi ambavyo viliwafanya wamlilie Mungu na kupigana vita. Walipigana kiroho, wakapigana kimwili. Mfano halisi ni vita vyao na Waamaleki “Wakati huo Waamaleki wakatokea, wakapigana na Israeli huko Refidimu. Musa akamwambia Yoshua, tuchagulie watu, ukatoke upigane upigane na Waamaleki; kesho nitasimama juu ya kilele kile, na ile fimbo ya Mungu nitakuwa nayo mkononi mwangu. Basi Yoshua akafanya kama Musa alivyomwambia, akapigana na Amaleki; na Musa na Haruni na Huri wakapanda juu ya kile kilima. Ikawa, Musa alipoinua mkono wake, Israeli waliposhinda; na aliposhusha mkono wake, Amaleki walishinda. Lakini mikono ya Musa ilikuwa mizito; basi wakatwaa jiwe, wakaliweka chini yake akalikalia. Haruni na Huri wakaitegemeza mikono yake, mmoja upande huu na mmoja upande huu; mikono yake ikathibitika hata jua lilipokuchwa. Yoshua akawaangamiza Amaleki na watu wake kwa ukali wa upanga. BWANA akamwambia Musa, Andika habari hii katika kitabu iwe ukumbusho, kisha ihubiri masikioni mwa Yoshua; ya kuwa nitaufuta ukumbusho wa Amaleki kabisa, usiwe tena chini ya mbingu. Musa akajenga madhabahu, akaiita jina lake Yehova-nisi; akasema, BWANA ameapa; BWANA atakuwa na vita na Amaleki kizazi baada ya kizazi.”  Kutoka 17:8-16

Wanadamu kwa jinsi ya ubinadamu wao wanaweza kufanya jitihada zao za kiganga na kichawi au za kawaida katika mwili wakakuwekea vipingamizi ili wewe mtu wa Mungu usiinuke. Lakini katika nguvu za Roho mtakatifu tutashinda na zaidi ya kushinda. Angalia mfano, Yesu Kristo walijaribu kumzuia asifufuke toka kaburini kwa kulilinda kaburi kwa kutumia askari wenye silaha na kuweka jiwe kubwa juu ya kaburi. “Hata siku ya pili, ndiyo iliyo baada ya Maandalio, wakuu wa makuhani, na Mafarisayo wakamkusanyikia Pilato, wakasema, Bwana, tumekumbuka kwamba yule mjanja alisema, alipokuwa akali hai, Baada ya siku tatu nitafufuka. Basi amuru kwamba kaburi lilindwe salama hata siku ya tatu; wasije wanafunzi wake wakamiba, na kuwaambia watu, amefufuka katika wafu, na udanganyifu wa mwisho utapita ule wa kwanza. Pilato akaawaambia, mna askari, nendeni mkalilinde salama kadiri mjuavyo. Wakaenda, wakalilinnda kaburi salama, kwa kulitia lile jiwe muhuri, pamoja na wale askari walinzi.” Mathayo 27:62-66
Lakini ilipofika saa ya Roho mtakatifu kudhihirisha nguvu zake, walinzi pamoja na silaha zao walikuwa kama wafu. Maandiko yanathibitisha; “Hata sabato ilipokwisha, ikapambazuka siku ya kwanza ya juma, mariamu Magdalene, na Mariamu yule wa pili, walikwenda kulitazama kaburi. Na tazama, palikuwa na tetemeko kubwa la nchi, kwa sababu malaika wa Bwana alishuka kutoka mbinguni, akaja akaliviringisha lile jiwe akalikalia. Na sura yake ilikuwa kama umeme na mavazi yake meupe kama theluji. Na kwa kumwogopa, wale walinzi wakatetemeka, wakawa kama wafu. Malaika akajibu, akawaambia wale wanawake, Msiogope ninyi, kwa maana najua ya kuwa mnamtafuta Yesu aliyesulibiwa. Hayupo hapa, kwani amefufuka kama alivyosema. Njoni, mpatazame mahali alipolazwa. Nanyi nendeni upesi, mkawaambie wanafunzi wake, Amefufuka katika wafu. Tazama, awatangulia kwenda galilaya; ndiko mtakakomwona. Haya nimekwisha waambia.” Mathayo  28:1-7

Roho Mtakatifu ni Nguvu ya Mungu na ni Pumzi ya Mungu yenye kuleta uhai tena. Kama Kristo alihamishwa toka kwa wafu nasi tutahamishwa kiroho na kimwili kwa nguvu za Roho Mtakatifu.

ROHO MTAKATIFU UFUNGUA VIFUNGO VYA UTASA;
Kwa nguvu za Roho Mtakatifu na uweza wake Sara alipokea uwezo wa kuwa na mimba alipokuwa amepita wakati wake. Milango na malango ya utasa yaliyomfunga Sara muda wa miaka wa ishirini na mitano, kwa imani ilifunguliwa.
Kwa imani hata Sara mwenyewe alipokea uwezo wa kuwa na mimba; alipokuwa amepita wakati wake; kwa kuwa alimhesabu yeye aliyeahidi kuwa mwaminifu.Waebrania 11:11
Hata sasa  kwa uwezo wa nguvu za Roho Mtakatifu, wako wakristo wengi watafunguliwa ndani mwa maombi ya kufungua milango na malango ya UTASA yasiwafunge tena maana yeye aliyeahidi ni mwaminifu na kusema, hatakuwepo mwenye kuharibu mimba wala aliye tasa katikati yetu.

Roho Mtakatifu akufunike kama kivuli wewe uliyekuwa umefunikwa na roho chafu za mashetani. Roho Mtakatifu na nguvu zake zikufunike kama kivuli, ili Vuli la uchawi na uganga litoke kwako. Kwa nguvu za Roho mtakatifu tumevishwa uweza na Kristo Yesu wa kufungua na kufunga na tutakachokifungua kitafunguliwa katika Mungu aliye hai. Na tutakachokifunga kitafungwa katika Mungu aliye hai. Maana maandiko yanasema;
 “Na ufungua wa nyumba ya Daudi nitauweka begani mwake; yeye atafungua wala hapana atakayefunga; naye atafunga wala hapana atakayefungua.” Isaya 22:22

Nguvu zake Roho mtakatifu zitakapokufunika, Utatenda makuu kwa uwezo wake. Katika yeye Roho Mtakatifu, Wagonjwa wanapokea uponyaji, wanaosumbuliwa na nguvu za mapepo wanawekwa huru mbali na mateso, walioshushwa chini na kudharauliwa wanainuliwa tena. “Akawaita wale Thenashara, akawapa uwezo na mamlaka juu ya pepo wote na kuponya maradhi.” Luka  9:1

Ni lazima tuhamishwe kwa Maombi yenye Imani. Usikubali kuteswa na kugandamizwa, Mtwike Yesu fadhaha zako, mizigo yako, taabu zako, vilio vyako  naye atakuhamisha tu.  Bwana atazitangua ishara zao wachawi na waganga, Maana kwa nguvu za Roho Mtakatifu hakuna uchawi wala uganga kusimama mbele yako tena. BWANA wa majeshi anasema; “Hakika hapana uchawi juu ya Yakobo, Wala hapana uganga juu ya Israeli.” Hesabu 23:23

Ushuhuda wa dada mmoja
Dada mmoja toka pale Kilimanjaro; alinijia akiwa na mateso ya magonjwa yaliyomkumba alipopigwa na upepo njia panda akiwa anakwenda dukani pale kijijini kwao. Baada ya kupigwa na upepo alianguka na kuzimia, alipozinduka alijikuta yuko hospitali akiwa amelazwa. Baada ya miaka miwili kupita tangu apigwe na upepo wa ajabu, ndipo alipokuja kwenye Ibada ya Maombezi ya kufungua Milango na Malango. Ndipo nilipomwombea kwa kuziita nguvu za Roho mtakatifu zenye kung’oa kila aina ya  mapando yaliyopandikizwa kwa watu wa Mungu. Hapa tunaona wachawi wanatumia upepo kumloga na kumwingia dada huyu. BWANA anatuma nguvu ya Roho mtakatifu katika kanisa la kwanza kama uvumi wa upepo. Maandiko yanathibitisha kwamba; “Hata ilipotimia siku ya Pentekoste walikuwako wote mahali pamoja. Kukaja ghafula toka mbinguni uvumi kama uvumi wa upepo wa nguvu ukienda kasi, ukaijaza nyumba yote waliyokuwa wameketi. Kukawatokea ndimi zilizogawanyikana, kama ndimi za moto uliowakalia kila mmoja wao.” Matendo ya Mitume 2:1-4

Upepo wa kichawi na kiganga uliokuwa unamtesa huyu dada ulimalizwa nguvu zake na kubatilishwa kwa Nguvu za Upepo wa Roho Mtakatifu, nikatengua kila aina ya upepo mchafu ulio mpitia kwa jina la Yesu Kristo.








No comments:

Post a Comment