Tuesday, March 19, 2013

Rev Florian Katunzi: Maombi hurejesha nguvu ya Uzima

Rev Florian Katunzi
KARIBU katika makala haya yanayoandaliwa na  hufundishwa na Mchungaji Florian J. Katunzi wa kanisa la EAGT City Centre, lenye makao yake viwanja vya Mwal. Julius Kambara Nyerere (Sabasaba) jijini Dar es Salaam. Wiki hii tukijifunza  kipengere kisemacho:    Maombi hurejesha nguvu ya Uzima. Endelea….
Biblia katika kitabu cha Yohana 11:1-46, inaonesha jinsi Yesu alivyoomba baada ya kufika katika kaburi la rafiki yake Lazaro. Bwana Yesu aliomba hivi:
“……Akainua macho yake juu, akasema, Baba nakushukuru kwa kuwa umenisikia… akalia kwa sauti kuu, Lazaro, njoo huku nje.”

Maombi ya Yesu Kristo yalikuwa tofauti na maombi ya Martha na Mariam dada zake Lazaro,wao waliomba na kuamini Lazaro watamwona siku ya mwisho, Yesu Kristo akaomba, kwa kuita kwa sauti kuu, Lazaro njoo huku nje.
Ile nguvu ya mauti ikasikia sauti ya maombi ya Yesu Kristo, nasi tuliomwamini Kristo tunayo mamlaka ya ki-Ungu ndani mwetu, yenye uwezo wa kugeuza mauti kuwa uzima.
Uwezo huu wa ki-Ungu tunakuwa nao pale tunapodumu ndani mwa maombi kwa kuwa tunavishwa nguvu ya kuvunja mafungo yote ya mauti na kuzimu.
Ushahidi wa kimaandiko unapatikana katika “Tazama, nimewapa amri ya kukanyaga nyoka na nge, na nguvu zote za yule adui, wala hakuna kitu chochote kitakachowadhuru.” Luka 10:17
Mauti inasikia sauti ya maombi, Mkristo mpendwa usipuuze maombi, Lazaro alitoka kaburini, si kwa Yesu kusimama mbele ya kaburi alimozikwa siku nne zilizopita,  bali, alipoomba, akatamka, akaita Lazaro toka nje, Lazaro akatoka nje, aliyekuwa amekufa akatoka ni mzima.
Ndugu zake Lazaro walisema ananuka, ameoza, lakini Yesu akasema ondoa jiwe. Hakuangalia harufu wala kuoza kulikoletwa na nguvu ya mauti na kuzimu.
Ni ukweli kuwa akili ya kibinadamu na hesabu za kisayansi zinaonesha kuwa mwili wa nyama ukishakosa oxygen na kulala kaburini kwa siku nne, ni lazima uoze na kunuka, ndugu wa Lazaro walikuwa na sababu zote za kuamini hivyo, lakini walisahau kuwa waliyekuwa naye  alikuwa ndiye uzima  na mauti haikuwa na nafasi kwake.
Yesu mwenyewe anasema: “….Usiogope mimi ni wakwanza na wa mwisho, na aliye hai; name nalikuwa nimekufa, na tazama, ni hai hata milele na milele. Nami ninazo funguo za mauti na kuzimu. (Ufunuo 1:17-18).
Hata wewe leo unaweza kuwa na tatizo kubwa  linalofanana na mwili wa Lazaro kaburini, ndugu jamaa  na rafiki wanakuaona kama uliyekwisha kabisa, unayesubiri ufufuo siku ya mwisho, lakini ndani mwa Maombi upo uzima wako, kama vile Mtumishi wa Mungu Ayubu alivyonena baada ya mateso na maumivu mazito.
Ayubu alisema hivi:
 “Watu wa mbari yangu wamekoma, na rafiki zangu niwapendao wamenisahau. Wakaao nyumbani mwangu na vijakazi vyangu, wanihesabu kuwa mgeni; mimi ni mgeni machoni pao. Namuita mtumishi wangu wala haniitikiii ingawa namsihi kwa kinywa changu. Pumzi zangu ni kama za mgeni kwa mke wangu name ni chukizo kwa ndugu zangu.
 Hata watoto wadogo hunidharau; nikiondoka, huninena. Wasiri wangu wote wanichukia; hao niliowapanda wamenigeukia. Mfupa wangu umegandamana na ngozi yangu na nyama yangu, nami nimeokoka na ngozi ya meno yangu tu….. laiti maneno yangu yangeandikwa sasa! Laiti yangeandikwa kitabuni! Yakachorwa katika mwamba wa milele, kwa kalamu ya chuma na risasi. Lakini mimi najua ya kuwa mteteaji wangu yu hai, na yakuwa hatimaye atasimama juu ya nchi. Na baada ya ngozi yangu kuharibiwa hivi, lakini, pasipokuwa na mwili wangu nitamwona Mungu; nami nitamwona mimi nafsi yangu, na macho yangu yatamtazama, wala si mwingine.Mtima wangu unazimia ndani yangu!”
Jambo la msingi hapa ni kuwa mtetezi wako yu hai hata kama unanuka, hata  kama umo kaburini, hata kama umeonekana umekufa kiuchumi, Yesu Kristo anayo nguvu ya kufufua pale tunamwomba; ndani mwa maombi tunapata uzima.
 Ukaniite siku ya mateso; nitakuokoa, na wewe utanitukuza,” Zaburi 50:15.
Ndani mwa Yesu Kristo imo nguvu ya uzima, yatupasa tukae ndani mwake pasipo kuzimia moyo.
Mpaka mifupa mikavu ikapokea uzima, si kwamba  Mtumishi wa Mungu Ezekieli aliomba siku moja tu,  urejesho ukatokea, hapana yalikuwa ni maombi endelevu.
BWANA ni mwaminifu pale tunaposimama katika maombi na anatuambia:
“Nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi BWANA, nitakapo yafunua makaburi yenu na kuwatoa ninyi katika makaburi yenu watu wangu. Nami nitatoa roho yangu ndani yenu, nanyi mtaishi …”
Mungu wetu anataka tujue kuwa  yeye ndiye atuwezeshaye; tumwishie kwa maombi ndani mwa maombi, maana uzima wa mtu haukufichwa katika mali alizo nazo.
Ustawi wa mtu haukufichwa katika fedha alizonazo, bali katika roho wa Mungu aliyemo ndani mwetu. Roho wa Mungu akiwa hai ndani mwetu; matokeo ya nje yataonekana.
Maandiko yanaonya sana, mtu wa Mungu kuishi bila kufuata taratibu za kiroho; kwa kutegemea upako wa mwili, lakini ndani mtu hana kitu.
“Basi, kama ni hivyo, ndugu, tu wadeni, si wa mwili tuishi kwa kufuata mambo ya mwili; kwa maana mkiishi kwa kufuata mambo ya mwili mwataka kufa; bali kama mkiyafisha matendo ya mwili kwa roho Mtaishi . kwa kuwa wote wanaoongozwa na Roho wa Mungu, hao ndio wana wa Mungu.  Kwa kuwa hamkupokea tena Roho ya utumwa iletayo hofu; bali mlipokea roho ya kufanywa wana, ambayo kwa hiyo twalia, Aba, yaani Baba. Roho mwenyewe hushuhudia pamoja na Roho zetu ya kuwa sisi tu watoto wa Mungu, warithio pamoja na Kristo; naam kuteswa pamoja naye, ili tupate kutukuzwa pamoja naye. Rumi 8:12-17.
Deni letu kwa Mungu ni kuwajibika ndani mwa maombi maana amtafutaye Mungu atamwona na amwitaye Mungu atamwitikia, hatuwezi kumwita Mungu nje ya maombi, bali ndani mwa maombi, hivyo inuka sasa uombe, ni wakati wa maombi.
Itaendelea…….

1 comment: