Friday, June 28, 2013

Jihadhari na Unafiki



Neno la Mungu katika Luka 16:15 “ Hapo akawaambia, Ninyi mnajifanya wema mbele ya watu, lakini Mungu anaijua mioyo yenu. Kwa maana kile kinachoonekana kuwa kitukufu mbele ya watu, Mungu anakiona kuwa takataka.”

Leo nimesukumwa niongee juu ya jambo hili linalotusumbua sisi Wakirsto na jamii kwa ujumla. Imekuwa kama kawaida siku hizi watu kuishi maisha ya unafiki.

Unafiki ni hali ya kutukuwa na maisha ya ukweli kwa kuwa na maisha ambayo hayana picha halisi ya kile kilichoko ndani ya moyo ya mtu.

Mtu mnafiki anafanya hivyo ili kupata sifa kwa watu wanamzunguka kama vile wachungaji,mabosi ofisini,marafiki na ndugu.

Mara nyingi lengo la mnafiki ni kuweka picha nzuri yake kwa watu huku akihakikisha kwa njia yoyote ile wengine wanaonekana wabaya.

Sio rahisi sana kumjua mnafiki maana anaweza kujifanya rafiki yako ili uwe wazi kwake apate nafasi ya kujua mtazamo wako ili aende kueleza kwa watu wengine kwa njia ya tofauti ambayo inakufanya uonekane mbaya.

Kama neno linavyosema hapo juu katika Luka 16:15 Mungu anajua mioyo ya wanafiki kwamba wanajifanya wema mbele za watu lakini hawako hivyo.

Pia katika Mathayo 6: 1“Angalieni msifanye wema wenu machoni pa watu, kusudi mtazamwe na wao; kwa maana mkifanya hivyo, hampati thawabu kwa Baba yenu aliye mbinguni.”  Neno linatuasa kabisa kutojifanya kwamba ni wema mbele za watu ili hali ndani ya mioyo yetu hatuna upendo nao,Mungu hatatupa thawabu kama tuna tabia hiyo.

Mtu mnafiki atakuja kukuambia hivi unajua wewe ni rafiki yangu sana yaani fulani kwakweli hakupendi kabisa,kumbe hapo anataka wewe useme kitu juu ya huyo fulani ili yeye akirudishe kwake.

Mnafiki mara nyingine anaweza kuwa chanzo cha uchonganishi na magomvi katika sehemu za kazi,makanisani na katika makundi mbalimbali,inaweza ikachukua muda sana kujua ni nani anayesababisha maana anakuwa ana picha nzuri kwa kila mmoja na anahakikisha kila mtu anamuona yeye ni mtu mzuri sana kumbe moyoni hamaanishi kabisaa.

Unafiki umesababisha mafarakano kwa ndoa,makanisani,kazini na katika familia pia.

Mnafiki anaweza kusababisha watu fulani wasipate haki zao kwasababu anakuwa ametumia wema wake ambao ni fake kuhakikisha anaharibu sifa za mwenzake labda kwa mambo aliyoanzisha yeye halafu akayageuza yaonekane kwamba mwenzake ndio ameyafanya au kusema.

Unaweza kuchukulia unafiki kwamba si dhambi ukaona kama vile ni kitu kidogo lakini tunajua neno la Mungu linasema dhambi zote ni sawa.

Hii tabia ya unafiki inaweza kusababisha hata kifo mpendwa kwa mfano kama mtu akaambiwa hayo yaliyosemwa na mnafiki na halafu akapata mshtuko unaomsababisha labda kupoteza maisha,sasa hapo yule mnafiki si atakuwa na mkono katika kifo hicho?

Kuna watu wamepoteza ndoa,kazi,ushirika makanisani,undugu na urafiki kwasababu tu kuna mnafiki mmoja alikwenda kuwazunguka.

Leo nimekuja kukumbusha kwamba tujichunguze wapendwa kama kuna hata mbegu ndogo tu ya unafiki ndani mwetu tutubu na tuache kabisa maana sio kusudi Yesu alilotuitia hapa duniani.

Tuwe makini tusije tukajisahau tukajikuta tumeingiwa na hii tabia ya unafiki,naomba tuombe Mungu atuwezeshe ili tuache kabisa kama tunayo maana Mungu ni mwaminifu na anasamehe dhambi.

Kuna mpendwa mmoja alishawahi kuingia kwenye tofauti na wakwe zake hakujua tatizo limeanzia wapi baadae ndipo alikuja kujua kuna rafiki yake wa karibu ndio alikua chanzo alifanya unafiki wake ndio ulisababisha yote hayo.Ilikuwa mbaya sana maana wote walikuwa ni wapendwa wazuri tu

Nimekupa huu mfano ili uone jinsi unafiki unavyoweza kuharibu mahusiano ya watu na kufanya watu wasiishi kwa furaha.

 Katika kitabu cha Mathayo 7: 17 Neno la Mungu linasema “Jihadharini na manabii wa uongo, watu wanaowajia wamevaa mavazi ya kondoo, walakini kwa ndani ni mbwamwitu wakali. Mtawatambua kwa matunda yao…..”

Katika msitari wa biblia hapo juu tunaona aina nyingine ya unafiki kutoka kwa watu ambao wanajifanya ni watumishi wa Mungu lakini kumbe sio,hii imechukua kasi sana hapa nchini na duniani kwa ujumla. Ashukuriwe Mungu aliyetupa Roho wake Mtakatifu ambaye ni mshauri maana ndio anaweza kutushauri ili tusije tukaingia katika mitego yao.

Ni maombi yangu hii roho ya unafiki iondoke katika makanisa na maisha yetu,wa kuindoa ni mimi na wewe kwa kujihadhari nayo kwa kushauriana,kuombeana na kulijaza neno la Mungu kwa wingi katika maisha yetu.

Mungu atusaidie maana peke yetu hatutaweza kujiepusha nahii roho ya unafiki.

No comments:

Post a Comment